Thursday, February 21, 2013

Mama aliyemtesa mtoto ahukumiwa

HATIMAYE haki imetendeka, hayo ni maneno waliyoyasema baadhi ya wakazi wa Mbeya waliohudhuria katika Mahakama ya Wilaya na kushuhudia Wilvina Mkandara (24) akihukumiwa kifungo cha maisha jela kutokana na kesi iliyokuwa inamkabili ya kumtesa hadi kumsababishia ulemavu mtoto, Aneth Johannes (4) aliyekuwa akimlea.


--> Mara baada ya hukumu hiyo kutolewa Jumatatu iliyopita na hakimu mkazi aliyekuwa akisikiliza kesi hiyo, Gilbert Ndeuruo, wananchi walionekana kufurahi na wengi wakitaka japo kumgusa mfungwa huyo mpya lakini ulinzi wa polisi ulikuwa imara.
“Huyu mama angenyongwa tu,” alisikika akisema mama mmoja aliyeonesha kuwa na hasira na mfungwa huyo aliyekuwa amezungukwa na askari polisi.

Akisoma hukumu hiyo iliyozusha cherekochereko kutoka kwa baadhi ya wakazi hao wa Mbeya mahakamani hapo, Hakimu Ndeuruo alisema mshitakiwa amehukumiwa kutokana na kifungu cha 235 cha mwenendo wa makosa ya jinai cha mwaka 1985.

Akaongeza kuwa mahakama hiyo imeona mshtakiwa anastahili adhabu kutokana na mtuhumiwa huyo kama mzazi kushindwa kujali afya ya mtoto wakati alikuwa mama mlezi ikiwa ni pamoja na kumpeleka hospitali kwa wakati ili apatiwe matibabu.

Hakimu Ndeuruo amesema mahakama hiyo haikuridhishwa na ushahidi wa utetezi wa mtuhumiwa alioutoa mahakamani kuwa majeraha yaliyokutwa mwilini mwa mtoto Aneth yalitokana na kuugua tetekuwanga, jambo ambalo alisema si la kweli.

Aidha, mshtakiwa Wilvina alipotakiwa kujitetea ili apunguziwe adhabu kabla ya kusomewa hukumu alisema: “Naiomba mahakama inipunguzie adhabu kwa kuwa mimi ni mjamzito pia sijui mwanangu niliyemzaa alipo kwani sina mawasiliano na familia yangu.”

Akitoa hukumu hiyo Hakimu Ndauruo alisema amesikitishwa na kitendo cha mtuhumiwa huyo kutotaka kujua alipo mtoto aliyemkosea na badala yake kumjali wake. Mwanamke huyo alipandishwa kizimbani kwa mara ya kwanza Novemba 16, mwaka jana.

No comments:

Post a Comment

Blogger Widgets